Tarishi Hauwawi

August 15, 2008

Utata wa malazi wanafunzi mlimani upo pale pale

Filed under: habari ndio hiyo — tarishi @ 11:41 am

Mwanzoni mwa mwezi ujao wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ambao wengi wao wanachukua masomo ya shahada ya uzamili waliokuwa wakiishi katika hosteli za Ubungo wanatakiwa wawe wamehama katika majengo ya hosteli hizo.

Wanafunzi hao takribani 220 wanaondoka katika majengo hayo kupisha walimu wao ambao wameshaanza kupatiwa vyumba viwili kwa kila mwalimu mmoja katika majengo hayo yenye vyumba 36 kwa kila jengo. Majengo hayo ni matatu.

Nilipofanya mahojiano na Ofisa Uhusiano wa chuo hicho cha elimu ya juu nchini, alinieleza lengo la kubadilisha matumizi hayo ni kuwasaidia walimu wao ambao kwa sasa wanakabiliwa na upungufu wa nyumba.

Uamuzi huo kwa upande mmoja ni mzuri unaoonyesha chuo kinawajali walimu wake lakini nikiangalia suala hilo kwa upana zaidi naomba kutofautiana na uongozi wa chuo hicho kwa kufikia uamuzi huo ninaouona unaweza kuwa na hasara zaidi ya faida.

Itambulike kuwa chuo hicho kinapokea wanafunzi wapya zaidi ya 5,000 kila mwaka wakiwamo 3,000 wanaosomea katika kampasi kuu ya chuo hicho. Wanafunzi hao wengi wanatoka mikoa mbalimbali ya Tanzania na wakifika Dar es Salaam wanakuwa wageni.

Kutokana na idadi kubwa ya wanafunzi wanaosoma chuoni hapo ambao idadi yake inatarajiwa kuendelea kuongezeka katika siku zijazo haiendi sambamba na uwezo wa malazi. Sasa hivi tunaelezwa kuna upungufu wa hosteli za wanafunzi wanaosoma chuoni hapo licha ya kuwapo baadhi ndani ya kampasi kuu na kule Mabibo.

Ikiwa leo uongozi wa chuo unaona busara kuongeza uhaba huo wa hosteli za wanafunzi kwa kuwaangalia zaidi walimu wao ni wazi ni uamuzi wa kibinafsi.
Uongozi wa chuo unaweza kusema si kazi yao kuangalia malazi ya wanafunzi lakini kulingana na mazingira halisi ya hapa kwetu ni wajibu wao kuhakikisha wanafunzi, hasa wanaotoka nje ya Dar es Salaam, wanakuwa na uhakika wa malazi katika kipindi chote cha masomo na si mwaka wa kwanza pekee.

Uamuzi huo wa kubadilisha matumizi ya hosteli hizo tayari umeongeza tatizo la wanafunzi takriban 220 kukosa malazi katika kipindi cha masomo kinachoanza Septemba na tatizo hili limekuwa likikua kutokana na uamuzi wa chuo kubadilisha matumizi ya hosteli za wanafunzi kama ilivyowahi kutokea kubadilishwa matumizi kwa hosteli za Kijitonyama.

Naamini kutatua tatizo la nyumba kwa walimu ni rahisi kuliko kuwapatia malazi wanafunzi kwani wao wakipatiwa posho za nyumba wana uwezo mkubwa wa kwenda mtaani kutafuta nyumba za kuishi na wakaendelea kufundisha chuoni hapo. Hali ni tofauti kwa wanafunzi ambao wengi wao si wakazi wa Dar es Salaam ambao itawagharimu zaidi kupanga chumba au kuweza kujikusanya na kupanga nyumba.

Wanafunzi wanatakiwa kukaa pamoja katika mazingira tulivu ili waweze kujisomea lakini leo wakizagaa mitaani kweli watasoma hao? Hivi tunawajengea mazingira ya kufanya vizuri masomo yao au tunawajengea mazingira ya kuharibikiwa na kuongeza wahuni badala ya wasomi?Nionavyo mimi UDSM iangalie zaidi kupunguza tatizo la hosteli za wanafunzi na si kulizidisha kwa kuwaangalia walimu wao pekee. Iwasaidie pia wanafunzi wao.

No Comments Yet »

No comments yet.

RSS feed for comments on this post. TrackBack URI

Leave a comment

Blog at WordPress.com.